
MIKE TYSON sasa yuko mbioni kuorodheshwa, kisha kutamkwa kuwa mmoja kati wale walio katika orodha ya mabondia wakuheshimiwa na kukumbukwa duniani.
Huku hili linatarajiwa kutamkwa rasmi baadae mwaka huu tayari baadhi ya wadau wa mchezo wa masumbwi duniani wameanza kulizungumzia, huku wakihoji juu ya uamuzi huo.
Lakini ukweli unabaki pale pale kuwa katika maswala ya masumbwi Tyson ataendelea kustahili milele, kwani bado anashikilia rekodi ya kuwa Bingwa wa Dunia wa masumbwi ya uzito wa juu akiwa na umri mdogo na huo aliupata katika miaka ya 1980.
Pamoja na ubingwa huo, Iron Mike pia amekuwa ni bondia maarufu sana katika historia ya wanamichezo duniani.
Wadau je mnakumbuka enzi za kusubiri masumbwi hadi saa kumi na moja za alfajiri pale Palm Beach hotel....palikuwa panaitwaje tena.....? 'SUGAR RAYS"Itakumbukwa kuwa baada ya kutumikia kifungo, kutokana na kosa la kubaka, Tyson alirejea ulingoni akiwa na nia moja tu ya kurejesha tena mikanda yake ya ubingwa wa dunia uzito wa juu.
Kipindi hicho kilipita huku mashabiki wa ngumi bila ya kujali atashinda au atashindwa walisubiri kwa hamu mapambano yake.
Nakiri kuwa wachache kati yetu watajisahaulisha yale mapambano mawili ya Tyson dhidi ya Evander Holyfield, kwa nia njema na mbaya.
Inagawa lile pambano alilochapwa na James 'Buster' Douglas miaka ishirini iliyopita kwa hakika, liliusitua ulimwengu na si la kusahaulika.
Kiutamaduni Mike Tyson,ambaye sasa ana umri wa maiaka arobaini a tatu (43),atabaki akikumbukwa sana duniani kwa mengi mazuri na mabaya kuliko mwanamichezo mwingine yeyote katika kizazi tunachoishi.
Sasa basi, kuhoji kwa wadau kunakuja baada ya kuangalia kile ambacho bondia huyu amekuwa akikifanya nje ya ulingo, mmoja wao akiwa ni Promota anayeheshimika sana nchini Uingereza na duniani Frank Warren.
Anasema ameshawahi kukutana na Tyson mara kadhaa na anachoweza kusema ni kuwa bondia huyu, mara nyingine huwa ni mchangamfu sana na utamfurahia lakini wakati mwingine unaweza kuogofywa naye.
Promota huyu anasema yale mabaya yasihesabiwe kwa Tyson na atangazwe kuwa mmoja wa mabondia bora waliowahi kuishi duniani na akahoji kwani Sonny Liston alikuwa malaika?
Wengi wengine waliohoji juu ya Tyson inaonekana wazi kuwa wanamhusisha na kashfa za ngono amabazo zimekuwa zikiwaandama wanamichezo kama John Terry, Ashley Cole na Tiger Woods.
Lakini vyovyote vile jamani katika ulimwengu huu, ni nani ambaye anaweza akasimama na kunyooshea kidole mwenzie kuwa ni mbaya wakati ana ya kwakwe ambayo hayajawekwa wazi tu.
Tyson hakuamka asubuhi na kuwa bondia mkali katika masumbwi, alifanya kazi ya ziada, alijituma akapambana na kufikia kuwa Bondia mdogo kuliko wote kutwaa ubingwa wa dunia uzito wa juu.